MWENYEKITI
wa Chama Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba amesema kuwa sababu za
kuwa na uchumi tegemezi zinachangiwa na kuongozwa na viongozi wabovu wanaoendesha
nchi kwa kutokuwa na dira.
Akizungumza
hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Profesa Lipumba ambaye ni mtaalamu wa
uchumi alisema uongozi bora ni jambo muhimu katika maendeleo ya kiuchumi.
Alisema kama
uongozi unakuwa mbovu hauwezi kuwa na dira ya kuweza kujenga uchumi usiokuwa
tegemezi ila utakachofanya ni kushiriki katika biashara.
Profesa
Lipumba alifafanua kwa kusema “Uchumi tegemezi ni ule ambao serikali haina
uwezo wa kuendesha shughuli zake za ndani ila kwa kupata misaada kutoka nje,”.
Akielezea
matatizo ya uchumi yanayolikumba taifa kwa sasa alisema ni matatizo yaliyoanza mwanzoni
mwa mwaka 1960 katika nchi nyingi za kiafrika kama Tanzani, Ghana, Guinea ambazo
zilikuwa na mikakati ya kujaribu kujenga ujamaa.
Anasema kuwa
katika ujenzi wa ujamaa Tanzania haikuweza kutoa fursa kwa wajasiliamali wa
ndani kuwawezesha kuwa wawekezaji na kuwawezesha kujua mbinu za kibiashara kwa
nia ya kuwawezesha kuongeza uzalishaji .
“Kwa mfano
hapa Tanzania mkulima aliyekuwa na ekari 10 alihesabika kama Bepari na Kabaila,
wakati heka hizo ni kidogo sana. Hali iliyosababisha kuwa na sera za kujenga
ujamaa wa vijijini ambapo wakulima wote walitakiwa kuwa na shamba la pamoja la ujamaa
ambalo lilitakiwa kuwa na manufaa kwa watu wote,”.
Anaongeza
kuwa sera hizo ziliondoa motisha kwa wakulima wadogowadogo kuwekeza katika
sekta ya kilimo ikiwamo kuweza kujiendeleza na kuweza kukuza kilimo chao.
Alisema kuwa
“Matatizo zaidi yalionekana mwaka 1970, ingawa kulikuwa na matatizo ya uchumi
wa dunia na kuanguka kwa bei ya bidhaa zetu ikiwamo kuongezeka kwa bei ya
mafuta hali iliyotufanye tujikute tumeingia katika matatizo makubwa ya ukosefu wa fedha za kigeni,”.
Alisema kuwa
baada ya kujikuta katika hali hiyo ilibidi kujikuta nchi ikiangukia katika mikono
ya mashirika ya Kimataifa ya Fedha hususani Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF),
Benki ya dunia kwa sababu nchi haikuwa na fedha za kigeni hivyo ikawa inahitaji
kupata misaada iweze kujiendesha.
“Tatizo hilo
liliendelea kwa muda mrefu na kusababisha kushindwa kujinasua na kujenga uchumi
ambao unatoa fursa kwa wananchi wenyewe kuwa wajasiliamali ili waweze kuwekeza
na hapo ndipo tukaacha kilimo pembeni na wakulima wadogowadogo bila msaada,”
alisema Profesa Lipumba.
Akielezea
kuhusu aina za utegemezi Profesa anasema kuwa ni utegemezi wa masoko ambao nchi
nyingi za Afrika zimekuwa zikizalisha mali ghafi na kuziuza katika nchi za
Magharibi ikiwamo na zile za Asia ya Mashariki.
Utegemezi
mwingine ni ule wa Teknolojia ambazo huagizwa kutoka nchi za nje na mwingine ni
ule wa mitaji kutoka kwa wawekezaji wa nje hasa katika sekta binafsi unafanyika
kwenye maeneo ya madini na viwanda.
Utegemezi
mwingine ni misaada ambayo huingia katika bajeti za serikali ambayo karibu theluthi
moja inategemea misaada kutoka nje pamoja na kujitawala katika miaka 52, nchi
imeshindwa kujinasua katika wimbi la utegemezi kutoka nchi za Magharibi.
Utegemezi
mwingine aliouzungumzia ni ule ambao hauepukwi wa kushirikiana katika kujenga
uchumi wa kisasa ambao ni kushirikina katika biashara na nchi zilizopiga hatua
katika Maendeleo makubwa.
“ili uweze
kuendelee lazima ushirikiana nazo ili uweze kujijengea uwezo, jambo ambalo
tumeshindwa ni kuweka mkakati wa kujenga uwezo wa ndani, wa kuweza kuwa na
viwanda vinavyotengeneza bidhaa kwa kuweza kuongeza thamani ya malighafi
tunazozalisha ndani ya nchi, na kuweza kutrumia vizuri rasilimali zetu na
kuweza kujiletea maendeleo, tumekuwa na udhaifu katika matumizi ya fedha za
umma, tumekuwa na udaifu katika ukusanyaji wa mapato ya serikali na kutumiwa
kwa tija ili kuongeza uzalishaji, kukipa kipaumbele kilimo cha mkulima mdogomdogo
ili aweze kuongeza uzalishaji kwa kuwa anakuwa soko la bidhaa za viwandani,”
alisema.



