![]() | |
| Dimaond kushoto akimkabidhi Muhidini Gurumo gari alilomnunulia. |
MKALI wa Bongo Flava nchini,
Naseeb Abdul, juzi alifanya uzinduzi wa video ya kibao chake kiitwacho My
Number One, iliyokwenda sambamba na kumkabidhi zawadi ya gari la kutembelea aina
ya Toyota Fun Cargo, mkongwe wa dansi aliyestaafu hivi karibuni, Muhidini
Maalim Gurumo.
Uzinduzi na makabidhiano hayo vilifanyika, kwenye Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam, ambapo Diamond Platinum
alikiri kutambua na kuthamini mchango wa wanamuziki waliomtangulia, akiwamo
Gurumo ndio maana akampa zawadi hiyo.
Gurumo aliyekuwa mwanamuziki
wa bendi ya Msondo Ngoma wiki iliyopita alitangaza kustaafu muziki akiwa na
umri wa miaka 73, ambapo amekuwa ndani ya tasnia hiyo kwa miaka 53 na kusema anastaafu
kutokana na umri, ingawa alikiri kumaliza zama zake akiwa hana hata baiskeli.
Ndipo Diamond alipofanya
uzinduzi na kukabidhi gari, ambapo baada ya kuzindua na kutambulisha rasmi
video yake ya ‘My Number One’, mkali huyo alitumia fursa hiyo kumkabidhi Gurumo
ambaye alikuwa mmoja wa waalikwa.
Akizungumza baada ya
kukabidhi gari hiyo yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni saba, Diamond
alisema kuwa anathamini mchango wa wanamuziki waliotangulia, kwa kuwa wao ndio chagizo
la wasanii wachanga na sanaa yao izidi kukua.
"Katika safari yangu ya
kimuziki nilikuwa nikitamani sana kuwa na jina na kutunga nyimbo kama baba
yangu Gurumo. Nampenda na wanamuziki wengine wote wa Tanzania, maana bila wao sisi
wa kizazi kipya tusingejua njia za kupita ili kufikia malengo,” alisema
Diamond.
Baada ya kukabidhiwa funguo
na kuambiwa dhamira ya kualikwa kwake, Mzee Gurumo alisema kuwa, hana neno
linalotosha kulezea hisia zake juu ya tukio hilo la kukabidhiwa gari
alilonunuliwa na msanii Diamond, ambaye ni msanii anayemkubali zaidi katika Bongo
Fleva.
"Namshukuru sana huyu
kijana (Diamond) kwa kitendo chake hiki ambacho ni cha kushtua na kushangaza
wengi, namuombea kwa Mungu ampe mafanikio makubwa zaidi katika tasnia ya muziki
wa kizazi kipya, ili aendelee kuwa juu zaidi," alisema Gurumo.
Gurumo aliyezaliwa mwaka
1940, alianza muziki mwaka 1960 na Bendi ya Kilimanjaro Chacha, kisha mwaka
1962 kuhamia Rufiji Jazz Band aliyofanya kazi kwa mwaka mmoja na kutimkia Kilwa
Jazz mwaka 1963.
Mwaka 1964 akawa mmoja wa
waasisi wa Nutta Jazz iliyobadili majina kadhaa kabla ya kuitwa Msondo Music,
ambapo mwaka 1978 aliihama na kuanzisha DDC Mlimani Park, kisha akatimkia
Orchestra Safari Sound na mwaka 1990 kurejea Msondo Music aliyostaafu nayo.
Na Salum Mkandemba

0 comments:
Post a Comment