MKUU wa mkoa wa Dar es Saalam, Said Meck Sadick amesema Watanzania
hawaaminiki Kimataifa kutokana na hivi karibuni kukamatwa kwa baadhi yao wakituhumiwa
kujihusisha na ufanyaji wa biashara za dawa za kulevya.
Hayo aliyasema jana, jijini Dar es Salaam alipokuwa akihutubia
mkutano wa wadau wa habari ulioandaliwa na Chama wa wanahabari wa Dar es Salaam
(DCPC), na kusema kuwa mwanzo wakati watanzania walipokuwa wakisafiri nje ya
nchi walikuwa wakiaminika kuliko watu wa mataiafa mengine.
Alibainisha kuwa doa ambalo limechangia kutoaminika
limetokana na kukamatwa kwa baadhi ya Watanzania wakijihusisha na biashara hiyo.
Aliongeza kwamba hapo mwanzo Watanzania hawakuwa
wakikaguliwa kwa kiwango cha juu kama ilivyo sasa kutokana na kuaminiwa kwao
ambako wakati mwingine haikuwalazimu kugongea viza zao hapa nchini bali
waliruhusiwa hata kugonga nje ya nchi.
Akizungumzia hatua za kuchukua kumaliza tatizo hilo alisema kwamba
vita hiyo haitaweza kufanikiwa iwapo itaachiwa ishughulikiwe na serikali peke
yake bali kila mtanzania ashiriki kuwafichua wafanyaji.
“Tunachotakiwa ni kuwaomba wanahabari na Watanzania
washirikiane na serikali kuwataja wale mapapa wanaowafahamu wakijishughulisha
na biashara hiyo ili wafikishwe katika vyombo vya sheria na kuchukulia hatua pindi
watakapopatikana na hatia,” alisema Mkuu huyo wa mkoa.
Akizungumzia kuhusu umuhimu wa wanahabari nchini Mkuu huyo
wa mkoa, anawaona kama nguzo muhimu kwa jamii kutokana na ukweli kwamba Wananchi
wengi wanawaamini kama ilivyo viongozi wa kidini.
Alisema iwapo wanahabari watatumia kalamu zao vibaya kwa
maslahi yao au ya mtu fulani wanaweza kujenga au kubomoa iwapo wataandika
habari isiyokuwa ya kweli.
Katika suala la mifarakano ya kidini, Mkuu huyo wa Mkoa
alikiri kuwepo na kuongeza kuwa imeshasababisha kutokea mapigano kwa baadhi ya
maeneo baada ya kuwepo kwa hali ya kutoelewana baina yao.
Alitoa wito kwa wanahabari kuepuka kuandika habari za
uchochezi ambazo zitaamsha hisia za makundi na kutugawa hasa kwa misingi ya
kidini kwani hata machafuko yanapotokea hakuna anayefaidika zaidi ya kupata
hasara..

0 comments:
Post a Comment