Social Icons

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Tuesday, December 24, 2013



Sudan Kusini yatimiza utabiri wa Nyerere

Bashir, Machar na Kiir
KATIKA moja ya hotuba zake, Rais wa Kwanza wa Tanzania, marehemu Julius K. Nyerere, aliwahi kusema kuwa, dhambi ya ubaguzi ni mbaya kama ilivyo tabia ya kula nyama ya mtu, kwamba ukianza kula nyama ya mtu, hutaacha.
Aliyasema hayo mwaka 1995 alipokuwa katika Hoteli ya Kilimanjaro (kwa sasa Hyatt Regency Dar es Salaam), jijini Dar es Salaam alipoonya juu ya madhara ya kutaka kuuchezea na hatimaye kuuvunja Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Tanzania.
Nyerere akasema, “Watu wazima wameuzungumza Muungano kwamba tuuvunje au uendelee. Mtu mwenye akili hawezi kufikiri Uzanzibari ni fahari.” Akasema kuwa, nje ya Muungano, kuna Wapemba na Waunguja. “Mtamaliza kutengana na Watanganyika, mara mtakuta kumbe sisi si Wazanzibari.”
Mwalimu Nyerere akasema, “Mtajikuta kuna Wapemba na Waunguja. Wapemba watapata msukusuko kidogo na mara mtakuta kuna Wazanzibari na Wazanzibara. Hamtakaa salama. Hamuwezi mkakaa salama baada ya kutenda dhambi ya kuwabagua watu wa nchi yenu ileile moja mkawaita wale wao na hao sisi. Dhambi ile haiishii hapo….”,
Tofauti na Mwalimu alivyokuwa akitabiria Tanzania, utabiri huo umetimia katika nchi mpya ya Sudan Kusini iliyojipatia uhuru wake, Julai 9, 2011.
Uhuru huo ni zao lililotokana na hatu ya Januari 2011 baada ya wakazi wa Sudan Kusini kupiga kura juu ya swali la kujitenga na Sudan wakaamua karibu kwa kauli moja kuwa nchi huru.
Sababu kubwa inayoelezwa ya kujitenga kwa nchi hiyo inaelezwa kuwepo kwa tofauti kubwa kati ya nchi hizo ni kwamba katika Sudan yenyewe idadi kubwa ya watu wamekuwa Waislamu na utamaduni wao una mchaganyiko wa tabia za Kiarabu na Kiafrika na wengi wakizungumza lugha ya Kiarabu.
Kumbe kusini kuna Waislamu wachache, wengi ni wafuasi wa dini za jadi na wengine wakiwa wakristo.
Ukizungumzia upande wa kiuchumi na elimu nchi ya kusini ilielezwa kuwa nyuma ukilinganisha na nchi ya kaskazini.
Shinikizo la kimataifa lilizidi kuuandama uongozi wa Bashir ambako mwaka 2001, viongozi wa Umoja wa Mataifa walitoa wito kufanyika kwa jitihada za kumaliza mgogoro na kuruhusu misaada ya kibinadamu na wafanyakazi wa kimataifa kutoa msaada kusini mwa Sudan.
Amani ilipatikana baada ya kusainiwa rasmi kwa Mkataba wa Amani jijini Nairobi kwa pande zote mbili na Januari 9, 2005 na al-Bashir alikubali mkataba wa amani uliomaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuiwezesha Sudan Kusini kupata haki ya kujitawala.
Lakini vita vingine vya ndani vilianza katika eneo la Darfur (Sudan Magharibi) na kutokea kwa mauaji mengi na kufanyika matendo ya kinyama dhidi ya raia hali iliyomfanya al-Bashir mpaka leo kukabiliwa na mashtaka mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai(ICC), kama mshtakiwa wa makosa ya jinai dhidi ya haki za binadamu.
Baada ya kutengana kwa sababu hizo na nyingine nyingi na baadaye kufanikiwa kupata uhuru wakagundua kuwa nchi hiyo lazima itawalike kwa kuchanganya viongozi wa makabila mawiliu makuwa ambayo ni Lou Nuer analotokea aliyekuwa Makamu wa Rais Riek Machar na kabila la Dinka analotokea Rais Silva Kiir.
Lakini baada ya kuingia madarakani chokochoko zilianza na baada ya kufanyika kwa uchunguzi iligunduliwa kwamba Machar alikuwa na nia ya kutaka kumpindua Rais Kiir hali iliyofanya Julai mwaka huu achukue uamuzi mgumu wa kumtimua wadhifa huo.
Baada ya kumtimua Machar alisahau kwamba nchi hiyo ilijengwa kwa misingi ya makabila mawili hivyo ndani ya jeshi kulikuwa na makananda wengi waliokuwa wakitokea katika kabila la kiongozi huyo.
Mara baada ya kumuondoa wanajeshi hao walilichukulia suala hilo sawa na kutengwa na hivyo kumuona Kiir kama msaliti wao kwa kutaka kutawala mwenyewe na kabila lake kwa kugawana keki ya taifa.
Wanajeshi hao waliamua kumuunga mkono Machar na kutangaza kuasi jeshi na kuingia msituni kwa nia ya kuung’oa utawala wa Kiir.
Wanajeshi hao kwa sasa wameshafanikiwa kuteka baadhi ya miji katika nchi hiyo hali inayoweonesha uwezekano wa kuzuka kwa mapigano makubwa zaidi na kufanya hali katika taifa hilo jipya changa kabisa duniani kutibuka kwa haraka ambapo hivi sasa maelfu ya raia wakihama nchi hiyo kwa kukimbia vita.
Inaripotiwa kwamba idadi ya vifo mpaka sasa imefikia 1,000 huku mapigano yakiendelea kwa zaidi ya wiki.
Machar ameapa kumuondowa Kiir madarakani na vikosi vyake tayari vimeuteka mji wa Bor ambao ni mji Mkuu wa jimbo lenye vurugu la Jonglei ukiwa kama kilomita 200, kaskazini mwa mji mkuu wa Juba na pia wameuteka mji wa Bentiu ambao ni mji mkuu wa jimbo muhimu lenye kuzalisha mafuta la Unity.
Serikali ya Juba imekiri kwamba waasi wamefanikiwa kuchukua udhibiti wa majimbo ya Joglei na Unity huku maelfu ya watu wakikimbilia katika Mako Makuu ya Umoja wa Mataifa (UN) kupata hifadhi.
Msemaji wa jeshi la Sudan Kusini Philip Aguer mpaka jana alisema kuwa serikali imechukuwa hatua kwa ajili ya kufanya mashambulizi ya kurejesha miji yao iliyotekwa na waasi.
Anasema kuwa wanajeshi wao wataukombowa mji mwa Bor kutoka kwa vikosi vya waasi ambao bado unadhibitiwa na vikosi vya Machar lakini wanajiandaa kuudhibiti tena.
Matamshi hayo yanaibuka licha ya kuwepo kwa juhudi za kidiplomasia za mataifa ya Afrika na wito kutoka Marekani, Uingereza na Umoja wa Mataifa wa kutaka kusitishwa kwa mapigano hayo.
Mratibu mkuu wa masuala ya misaada ya kibinaadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini Toby Lanzer ameutembelea mji huo wa Bor juzi na kusema kwamba hali inazidi kuwa mbaya.
Amesema kuna maelfu ya raia wa Sudan Kusini waliokimbilia vichakani au kurudi kwenye vijiji vyao ili kuepuka madhara.
Ameongeza kusema ana wasi wasi mkubwa wa vita vinavyounyemelea mji huo ambapo amekiri kwamba ni jambo lisilofikirika kwa wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa kuwa katika uwezo wa kuwalinda raia wanaokadiriwa kufikia 15,000 wanaotafuta hifadhi katika kambi ya UN iliyoko huko.
Kwa mujibu wa Lanzer raia wa Australia,Uganda na Ethiopia ni miongoni mwa watu wanaotafuta hifadhi katika kambi ya UN huko Bor.
Ofisa huyo mwandamizi wa UN pia amesema helikopta za kiraia zimewahamisha raia wa Marekani kutoka mji huo ulioshuhudia mashambulizi mazito ya bunduki za rashasha lakini kuna raia 3,000 wa nchi kama vile Canada,Uingereza na Kenya wameendelea kuwaondoa katika mji huo.
Lanzer ambaye anatafuta msaada wa kifedha wa haraka kutoka Jumuiya ya Kimataifa amesema idadi ya wakimbizi wa ndani ya nchi inaweza kupindukia na kufikia 100,000.
Rais Barack Obama wa Marekani mwishoni mwa wiki ametuma barua kwa viongozi wa bunge la nchi hiyo akiwajulisha kwamba huenda akachukua hatua zaidi za kijeshi Sudan Kusini ili kuwalinda raia wa Marekani, wafanyakazi na mali zao.

0 comments:

 

Sample text

Sample Text

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sample Text