BAGHDAD, Iraq
MASHAMBULIZI kadhaa ya mabomu
yametokea nchini hapa na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 50 na wengine kujeruhiwa.
Polisi nchini humo wanasema kuwa
mashambulizi hayo yalilenga ngome za Waislamu wa madhehebu ya Kishia wakati
walipokuwa katika harakati za kwenda kazini huku wengine wakijishughulisha na
mambo mengine.
Kiwango cha machafuko kimeongezeka
nchini Iraq katika siku za hivi karibuni kutokana na uhasama unaoendelea
kukithiri kati ya Waislamu wa Kishia na wale wa Wasunni.
Polisi wanasema kuwa zaidi ya milipuko
10 ya mabomu ilitokea wiki iliyopita katika maeneo mbalimbali ikiwemo Wilaya ya
Jisr Diyala mjini Baghdad na mji wa Sadr.
Hadi sasa hakuna kundi lililojitokeza
kusema kujihusisha na mashambulizi hayo lakini polisi wanashuku kuwa
yalitekelezwa na wapiganaji wa Kisunni.
Waislamu wa Kisunni wanasema kuwa
wanatengwa na serikali ya Waziri Mkuu Nouri Maliki ambaye anaongoza serikali ya
Kishia tuhma ambazo serikali inapinga na kusema kuwa wapiganaji hao wanatumiwa
na makundi ya kigaidi.
Tangu kuanza kwa mwaka huu, zaidi ya
watu 4,000 wameuawa na wengine 10,000 kujeruhiwa kutokana na mashambulizi hayo
ya mabomu.
Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha
kuwa Julai ilikuwa mbaya kwa raia wa Iraq baada ya watu 1,057 kupoteza maisha
yao wengi wao wakiwa mjini Baghdad.
REUTERS
Mwisho.
Operesheni ya kijeshi
yanukia Syria bila UN
DAMASCUS, Syria
UWEZEKANO wa Umoja wa
Mataifa (UN), kuidhinisha mashambulizi dhidi ya Syria ni mdogo sana, lakini
tayari Marekani na washirika wake wanafanya maandalizi ya mashambulizi kupitia
dhana ya uwajibikaji wa kimaadili.
Wiki moja baada
kutokea shambulio linalodaiwa kuwa la kemikali kufanywa nchini Syria, mataifa
kadhaa yameanza kupeleka vikosi kujiandaa na mashambulizi dhidi ya serikali ya
Rais Al Assad.
Mwanzoni mwa wiki
Waziri wa mambo ya kigeni wa Uingereza William Hague alielezea uhakika kwamba
gesi ya sumu ilitumiwa na vikosi vitiifu kwa rais Assad.
Tukio hilo
linaendelea wakati uchunguzi wa karibu juu ya shambulio hilo unaendelea
kufanywa na wakaguzi wa Umoja wa Mataifa.
Vikosi hivyo
vinasubiri kauli ya wachunguzi wa Umoja wa Mataifa ambao iwapo watabainisha
kuwa gesi hii ya sumu ilitumiwa na upande wa serikali, hakuna kitakachozuia
mashambulizi ya kijeshi.
Muungano wa hiari
Kulingana na muktadha
wa sheria hata hivyo, mashambulizi hayo yatakuwa yanakiuka sheria za kimataifa,
kwa kuwa uhalali wake unaweza kutokana na baraza la usalama la Umoja wa
Mataifa, ambako China na Urusi zinaweza kuzuia mpango huo kwa kutumia kura zao
za turufu.
Kwa nchi hizo mbili,
uingiliaji kijeshi kutoka mataifa ya nje siyo njia ya kuleta suluhu.
Kama litafanyika shambulizi
la kijeshi, haitakuwa mara ya kwanza kwa Marekani kuchukua hatua kama hiyo
pasipo idhini ya Umoja wa Mataifa kwani hata wakati wa utawala wa Rais wa
zamani wa Marekani George W. Bush, kupitia kile alichokiita muungano wa hiari,
aliyaongoza mataifa kadhaa kuivamia Iraq mwaka 2003, kwa madai ya kuikomboa
kutoka mikononi mwa Saddam Hussein.
Kabla ya uvamizi huo,
Marekani ilijaribu kupitisha hoja yake ndani ya baraza la usalama la Umoja wa
Mataifa, kuonyesha kuwa kulikuwepo silaha za maangamizi nchini Iraq, ambapo
waziri wa ulinzi wa wakati huo Collin Powell aliwasilisha ushahidi wa madai
hayo katika baraza.
Hata hivyo, kulikuwa
na mashaka makubwa kwa upande wa Ufaransa, Urusi na Ujerumani kuhusiana na
ushahidi huo, na waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Joschker Fischer,
alieleza bayana kuwa hakuridhika na ushahidi wa Marekani.
Na kwa hakika mashaka
yake yalikuja kutimia, baada ya kubainika kwamba ushahidi uliyowasilishwa
katika umoja wa mataifa ulikuwa wa kughushi na Collin Powell alikiri kufanya
makosa na kujiondoa katika ulingo wa siasa.
Waziri mkuu wa
Uingereza David Cameron anakutana na maofisa wa juu wa serikalini na jeshi
kujadili mikakati.

0 comments:
Post a Comment