Social Icons

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Thursday, September 12, 2013

Changanyikeni waandamana hadi Dawasco

DIWANI wa kata ya Makongo, Deusdedit Mtiro ameungana na wakazi wa eneo la Changanyikeni na kwenda Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasco), kutoa malalamiko yao ya kukosa maji kwa muda wa miaka saba.
Malalamiko hayo waliyepeleka jana katika ofisi za Dawasco Kimara, jijini Dar es Salaam kwenye ofisi za Meneja wa ofisi hiyo, Rukia Bachu.
Diwani Mtiro alianza kumueleza malalamiko yao Meneja huyo, Rukia kuwa Wananchi wa eneo la Changanyikeni wamekuwa katika tabu ya kukosa maji tangu mwaka 2006 hadi sasa.
Diwani Mtiro alisema “Nakumbuka mwaka 1989 tulikuwa tukipata maji vizuri, kupitia bomba ambalo tulikuwa tumelinunua kwa nguvu za wananchi, lakini mwaka 2006 mambo yalibadilika baada ya Dawasco kufunga mabomba ya Mradi wa Wachina, ndipo tulikosa maji mpaka leo,”.
Naye Mkazi wa eneo hilo Erick Mchata alisema kuwa wamekuwa wakifika mara kwa mara katika ofisi hizo ikiwamo Makao Makuu Dawasco lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika kwa ajili ya kutatua tatizo lao.
Mkazi mwingine, Mzee Kamba anasema anashangaa pamoja na kukosa maji kwa muda lakini amepelekewa bili ikionesha anadaiwa sh 1,000,000.
Kwa upande wa Mengyason Masawe alisema kuwa anaumia kuona maeneo yaliyo juu yao wanapata maji lakini wao wakikosa hata kwa siku moja kwa wiki.   
Akizungumzia malalamiko hayo Meneja wa Dawasco wa Kimara, Rukia Bachu alikiri kuwepo kwa tatizo la kukosekana kwa maji katika eneo hilo kwa muda mrefu.
Akielezea sababu ya kuwepo kwa tatizo hilo anasema kuwa “Tatizo kubwa eneo hilo limekuwa likichangiwa na baadhi ya watu kumiliki matenki yenye ujazo mkubwa kiasi cha kusababisha wengine kukosa, hivyo ninawaomba mtusaidie kuwafichua wanaofanya mchezo huo ili kuwezesha kutatua tatizo hilo,” alisema Rukia. 
Meneja Rukia aliwaahidi kulishughulikia tatizo hilo na kuwawezesha wananchi hao kupata maji siku ya jumamosi ambako atamtuma mhandisi kwenda kuwaunganishia maji hayo ikiwa ni pamoja na kuwezesha kuwafichua wale wanaotumia matenki makubwa.


0 comments:

 

Sample text

Sample Text

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sample Text