Waajiri watii sheria ya ajira kwa watu wenye ulemavu
WAAJIRI wameshindwa
kutii sheria ya ajira ya mwaka 2010 inayowataka wale wenye wafanyakazi zaidi ya
20, wahakikishe asilimia tatu ya wafanyakazi wao wawe watu wenye ulemavu (WWU).
Hayo
yamebainishwa jana, Dar es Salaam na Meneja Programu ya utetezi Fredrick
Msigallah, wakati akiwasilisha mada yake kwenye uzinduzi wa ripoti za utafiti
kuhusu Ajira kwa watu wenye ulemavu uliofanywa kwa kushirikiana na Taasisi ya kusaidia walemavu ya (CCBRT) na
Radar Development.
Akiwasilisha
mada hiyo, Msigallah alisema katika utafiti huo walizishirikisha sekta binafsi
kutoka mikoa ya Arusha, Mwanza, Kilimanjaro, Morogoro na Tanga kwa kushirikiana
na Chama Cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na
Fedha (TUICO), ukiwa umezihusisha jumla ya kampuni 72 zilizo na wafanyakazi 50.
Akiwasilisha
alisema kuwa tathmini yao inaonesha idadi ya watu wenye ulemavu katika sehemu
za kazi bado iko chini.
Akithibitisha
hilo anasema kwamba katika Kampuni hizo zilizofanyiwa utafiti zinaonesha kati
ya wafanyakazi 20,568 ni wafanyakazi 86 pekee ambao ni asilimia 0.4 ndiyo wenye
ulemavu.
Anaongeza
kuwa kati ya Kampuni hizo 72 zilizofanyiwa utafiti huo ni mbili pekee
zilizofikisha zaidi ya asilimia tatu ya wafanyakazi wenye ulemavu na hivyo
kukidhi matakwa ya sheria ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2010 inayomtaka bayana
kuwa kila mwajiri mwenye wafanyakazi zaidi ya 20 ni asilimia tatu ya
wafanyakazi hao wawe wenye ulemavu.
Akielezea
sababu inayochangia kutokea kwa tatizo hilo Msigallah alisema “Utafiti unaonesha
kuwa waajiri wengi hawana uelewa wa kutosha kuhusu sheria hiyo na sera
zinazosimamia masuala ya ajira kwa watu wenye ulemavu, kwani kati ya kampuni
zilizofanyiwa utafiti ni asilimia 40 pekee viongozi wake walionesha kufahamu
sheria na sera zinazohusu ajira kwa watu wenye ulemavu,”alisema Msigallah.
Akielezea utafiti
walioufanya katika sekta ya elimu wakiwa wameshirikiana na Chama cha Walimu
Tanzania (CWT), ukiwa umelenga walimu wa msingi sekondari na vyuo wa mikoa ya
Dar es Salaam, Mara, Lindi, Mbeya, Singida na Tabora ambako walibaini kuwa kuna
walimu 24,552 na wale waliokuwa na ulemavu walikuwa 519 ambao ni asilimia 2.1
pekee.
Msigallah
aliongeza kuwa utafiti huo ulibaini kuwa walimu wenye ulemavu wanaopata nafasi
za uongozi ni ndogo huku wengi wao wakiwa wanaume ambako wale wenye nafasi ya
mwalimu mkuu walikuwa 519 na miongoni mwao asilimia 79 ni wanaume na asilimia
21 ni Wanawake.
Katika sekta
ya Afya, anasema walifanya utafiti kwa kuwashirikisha Wizara ya Afya na Ustawi
wa jamii kupitia Idara ya Ustawi wa Jamii walibaini miongoni mwa wafanyakazi
738 ni 17 pekee ndio walikuwa wenye ulemavu na miongoni mwa hao ni asilimia
64.7 walikuwa wanaume na wanawake asilimia 35.3.
Naye
Mkurugenzi wa Ajira wa Wizara ya Kazi na Ajira, Ally Msaki, alikiri kuwepo kwa changamoto
nyingi zinazochangiwa na historia ya kiimani na kitamaduni.
Msaki
anasema changamoto nyingine ni namna ya kusimamia utekelezaji ambao hata hivyo
hivi sasa serikaliu imeanza kwa kufanyika utafiti mkubwa kwa kupitia Ofisi ya
Taifa ya Takwimu ili kujua mahitaji mbalimbali ikiwamo ajira kwa watu wenye
ulemavu.
Alisema kuwa
njia ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata ajira kwa kupitia sheria ya
mwaka 2010 ni kufikiria kutoa motisha na elimu kwa waajiri.
“nitahakikisha
nashirikiana na viongozi wenu katika kuhakikisha tunafanikiwa katika suala hilo
la ajira,” alisema.
0 comments:
Post a Comment