Al-Shabaab yadai mateka 137
wamefariki
KUNDI la Al-Shabaab limedai kuwa mateka 137 waliowachukua
wamefariki katika uvamizi wa kituo cha biashara, idadi ambayo ni vigumu
kuithibitisha na kubwa kuliko idadi iliyotangazwa kuwa hawajulikani walipo.
Wapiganaji hao walio na mafungamano na mtandao wa Al-Qaeda,
katika ujumbe waliouweka katika mtandao wa kijamii wa twitter, walisema mateka
137 waliokuwa wanashikiliwa na mujahedeen walikufa.
Waliwashtumu pia wanajeshi wa Kenya kwa kutumia vifaa vya
kemikali kukomesha mkwamo huo uliodumu kwa siku nne.
"Katika hatua ya uoga wa dhahiri, vikosi vya Kenya kwa
makusudi vilitumia kemikali," ulisema ujumbe mmoja na kuongeza kuwa, “ili
kufunika uhalifu wao, serikali ya Kenya iliendesha zoezi la kuliporomosha
jengo, na kuuzika ushahidi na mateka wote chini ya vifusi."
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, alitangaza kumalizika kwa
umwagaji huo wa damu uliodumu kwa saa 80 jioni ya Jumanne, ambao ulisababisha
vifo vya raia 61 na maofisa sita wa vikosi vya usalama.
Polisi ilisema idadi hiyo ya vifo ingeweza kuongezeka,
ambapo shirika la misaada la Msalaba mwekundu lilisema kuwa ni watu 63 ambao
bado hawajulikani walipo.
Hakukuwa na kauli kutoka serikali ya Kenya kuhusiana na
madai hayo, lakini Al-Shabaab wamekuwa wakitoa madai ya ajabu huko nyuma, hasa
kupitia akaunti yao kwenye mtandao wa twitter.
Kundi hilo lilisema lilifanya shambulizi hilo katika
kulipiza kisasi dhidi ya Kenya kutokana na kujiingiza nchini Somalia kupambana
na wanamgambo hao.
Katika moja ya mashambulizi yaliyofanywa katika historia ya Kenya, wapiganaji hao waliingia katika jengo la maduka la Westagate lenye ghorofa nne, ambalo linamilikiwa kwa sehemu na raia wa Israel.
Katika moja ya mashambulizi yaliyofanywa katika historia ya Kenya, wapiganaji hao waliingia katika jengo la maduka la Westagate lenye ghorofa nne, ambalo linamilikiwa kwa sehemu na raia wa Israel.
Kenya ilianza siku tatu za maombolezi rasmi jana, ambapo
bendera za taifa zinapepea nusu mlingoti, huku wafanyakazi wa uokozi
wakisafisha mabaki ya jengo la Westgate kutafuta miili ya wahanga wa tukio
hilo.
Karibu watu 200 walijeruhiwa katika uvamizi huo wa siku nne,
ambao ulishuhudia mapambano makali kati ya wapiganaji na vikosi vya usalama vya
Kenya katika jengo hilo, ambalo ndicho kituo kikubwa zaidi cha biashara na
maarufu kwa watu wenye uwezo nchini Kenya, wanadiplomasia, wafanyakazi wa Umoja
wa Mataifa na watalaamu wengine.

0 comments:
Post a Comment