Obama aomba idhini ya bunge
kuipiga Syria
WASHINGTON, Marekani
![]() |
| Rais Barack Obama kushoto na Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameroon |
ZIKIWA zimekatika zaidi ya
wiki, Ikulu ya Marekani imekuwa ikielekeza mashambulizi yake kuelekea kuchukua
hatua za kijeshi dhidi ya nchi ya Syria, lakini hayo yamebadilika baada ya rais
wa nchini hapa Barack Obama kutaka sasa baraka za bunge kuidhinisha hilo.
Uamuzi wa Rais Barack Obama
wa ghafla wa kuomba ruhusa ya bunge unamuweka katika hatari ambayo inaweza
kuharibu hali yake ya kuaminika iwapo hakuna hatua itakayochukuliwa kujibu
shambulio la silaha za kemikali ambalo limekiuka kile binafsi alichokiita kuwa
ni kuvuka ‘mstari mwekundu’.
Obama kuomba ruhusa ya baraza
la wawakilishi ambalo linadhibitiwa na chama cha Republican na baraza la seneti
linalodhibitiwa na chama chake cha Democratic kukubali kuchukua hatua za
kijeshi, suala ambalo tayari linaonesha utata ndani na kati ya vyama hivyo, inaifanya
hali hiyo kuwa tete kuhusiana na jibu la Marekani katika mzozo wa Syria.
Mabadiliko hayo ya ghafla yanazusha
maswali juu ya uwezo wa maamuzi wa rais na inaweza kuwafanya viongozi wa nchi hasimu
za Marekani kama Syria, Iran, Korea ya kaskazini na kwingineko, kuvimba kichwa na
kusababisha kujua kwamba rais wan chi hiyo hana nguvu ya kufanya jambo pasipo
kupewa ruhusa.
Bunge la Marekani hata hivyo
halitarajiwi kufanya vikao mapema mpaka Septemba 9, hali inayoonesha kwamba
suala la Syria litakuwa la muda mrefu huku mauaji yakiendelea katika nchi hiyo.
Hakuna mtu ambaye analijua
baraza hilo la Congress vizuri ambaye alikuwa tayari kutabiri kwa uhakika kile
kinachoweza kutokea katika azimio la kuiruhusu nchi hiyo kuishambulia Syria
lakini hali ya kutiliwa shaka inachangiwa kwa kiasi kikubwa na uhusiano mbaya uliopo
kati ya Obama na bunge la nchini mwake.
Ufaransa yapata kigugumizi
Kama ilivyo kwa Marekani hata
rais wa Ufaransa, Francois Hollande pamoja na kusema kuwa atamuunga mkono
Marekani kuiadabisha Syria kijeshi naye hana ubavu wa kuiunga mkono nchi hiyo
na kwenda vitani pasipo kupewa idhini na bunge lake.
Rais wa Urusi
Naye Rais Vladimir Putin wa
Urusi anaziona tuhuma zinazotolewa na Marekani na washirika wake kuhusu serikali
ya Syria kutumia silaha za kemikali ni za kipuuzi na hazina mashiko.
Anasema kuwa ni ngumu kulishutumu
jeshi la Syria kutumia silaha hizo za sumu wakati tayari lilikuwa linasonga
mbele na kutwaa maeneo yote yaliyokuwa yametwaliwa na waasi.
Putin alisema ikiwa Marekani
ina ushahidi kuthibitisha tuhuma zake, basi ikabidhi ushahidi huo kwa Baraza la
Usalama la Umoja wa Mataifa.
Alimkumbusha Rais Obama kuwa
aliwahi kutunzwa tuzo ya amani ya Nobel, na alimsihi kuwakumbuka wanyonge
katika mashambulio na alikaribisha uamuzi wa bunge la Uingereza ambalo
halikuunga mkono Uingereza kuingilia kati Syria, na anasema alishangazwa na
uamuzi huo wa busara wa bunge.

0 comments:
Post a Comment