Siku tatu za
maangamizi ya Al shabaab Westgate
KAMA kuna jambo ambalo kwa sasa linatikisa Afrika Mashariki
na dunia kwa ujumla ni hili la vikosi vya al Shabaab kushambulia na kuteka raia
waliokuwa kwenye jengo la kibiashara maarufu kama ‘Westgate’ nchini hapa.
Hadi jana vikosi vya usalama nchini Kenya vinasema
vimelidhibiti jengo zima la Westgate mjini Nairobi, ikiwa ni zaidi ya siku tatu
baada ya jengo hilo kuvamiwa na wanamgambo.
Hadi jana asubuhi kulisikika milipuko ikifuatiwa na milio ya
risasi kutoka ndani ya jengo hilo huku duru zikisema kuwa vikosi vya usalama
vinaelekea kukamilisha operesheni hiyo.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari, magaidi sita waliokuwa
wamebaki wameuawa na wengine watatu wakiwa wameuawa jana.
Serikali imesema zaidi ya watu 60 wameuawa na wengine zaidi
ya 170 kujeruhiwa katika shambulio hilo ambalo Al shabaab imekiri kulitekeleza.
Wizara ya Mambo ya ndani imesema wanajeshi wanaendelea
kulisaka jengo zima la Westgate kutoka ghorofa moja hadi nyingine kuhakikisha
kwamba hakuna mateka aliyebakia.
Wakati huohuo, waziri wa mambo ya nje amesema kuwa wawili
kati ya wanamgambo watatu waliofanya shambulio hilo ni raia wa Marekani pamoja
na mwanamke mmoja Muingereza.
Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni nchini
Marekani, Amina Mohamed alisema kuwa Wamarekani walikuwa kati ya umri wa miaka
18 na 19 wenye asili ya kisomali na waliishi mjini Minnesota.
Mshtakiwa mwingine alikuwa mwanamke Muingereza ambaye
inasemekana alikuwa amefanya vitendo vingi vya aina hii kwa niaba ya Al
Shabaab.
Mpaka sasa inaelezwa na shirika la Red Cross kuwa watu 63,
hawajulikani waliko.
Operesheni hiyo iliendelea usiku kucha ingawa kwa mujibu wa
waziri wa usalama wa Kenya, ilikuwa katika hatua za mwisho na mateka wote
wamefanikiwa kuokolewa.
Ruto apata afueni ya
muda
Tatizo hilo lilimuwezesha Makamu wa Rais wa Kenya William
Ruto kupewa ruhusa ya wiki moja na Jaji wa Mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa
kivita (ICC), kwa ajili ya kurejea nyumbani kushughulikia hali ya kiusalama
inayokumba taifa hilo.
Ruto na Rais Uhuru Kenyatta, wanakabiliwa na tuhuma za za uhalifu
dhidi ya binadamu baada ya kudaiwa kuhusika na ghasia za kikabila baada ya
uchaguzi wa mwaka 2007-2008 ambapo watu zaidi ya elfu moja waliuawa.
Kauli ya Marekani
Rais Barack Obama amempigia simu rais wa Kenya, Uhuru
Kenyatta na kumpatia pole kwa niaba ya Wananchi wa Marekani kutokana na
shambulizi walilofanyiwa na magaidi wa Ala Shabaab.
Taarifa ya Ikulu ya Marekani imeeleza kuwa Obama amemuahidi
Uhuru kumuunga mkono katika jitihada za kuusambaratisha mtandao wa kundi la
waislamu wenye msimamo mkali la al-Shabab.
Kundi hilo la al Shabaab limesema kuwa limefanya shambulio
hilo kwa nia ya kulipa kisasi cha kupigwa na kuondolewa katika nchi ya Somalia
wakati walipokuwa wameukalia mji wa Somalia mwaka 2011.
Nini na nani Al
Shabaab?
Al-Shabab ni neno la kiarabu linalomaanisha Kijana.
Kundi hilo liliibuka kama tawi la vijana la muungano wa
mahakama za kiislamu ambao baadaye muunganiko huo ulivunjika mwaka 2006.
Kuvunjika huko kulitokana na mapigano yaliyotokea baina ya
wanajeshi wa Ethiopia waliokuwa wameingia nchini Somalia kuunga mkono serikali
iliyokuwa dhaifu.
Kundi hilo likiwa Somalia liliweka sheria kali za kiisilamu
katika maeneo ambayo linadhibiti ikiwemo wazinifu kupigwa kwa mawe hadi kufa na
kutokubali mambo ya ndoa za jinsia moja (ushoga).
Je Al Shabaab
linadhibiti sehemu gani ya Somalia?
Ingawa kundi hilo limepoteza udhibiti, wa miji mikubwa, bado
linakita mizizi katika maeneo ya mashina.
Lililazimika kuondoka katika mji mkuu Mogadishu, Agosti mwaka
2011 na pia kuondoka katika mji wa bandarini wa Kismayo Septemba mwaka 2012.
Kismayo ulikuwa mji muhimu kwa kundi hilo, ambao ulikuwa
unawezesha bidhaa kuwafikia wapiganaji wa kundi hilo pamoja na kuwatoza watu
ushuru kwa shughuli zao.
Hizi ni silaha za Al Shabaab walizonasa wanajeshi wa AU
Muungano wa Afrika, ambao unaunga mkono juhudi za majeshi ya
serikali, ulisherehekea ushindi huo ingawa al-Shabab hufanya mashambulizi ya
mara kwa mara ya kujitoa mhanga mjini Mogadishu na kwingineko.
Wadadisi wanaamini kuwa al-Shabab limeanza kufanya
mashambulizi ya kuvizia baada ya kushindwa na majeshi ya Muungano wa Afrika
wanaotumia nguvu dhidi yao.
Lakini linakabiliwa na tisho kubwa kutoka kwa wanajeshi wa
Kenya walioanza harakati zao dhidi ya kundi hilo kuanzia mwaka 2011.
Kenya ilituhumu wapiganaji wa al-Shabab kwa kuwateka nyara
wanajeshi wake pamoja na watalii na sasa wamekuwa katika msitari wa mbele
kupambana na kundi hilo.
Nani kiongozi wa
al-Shabab?
Ahmed Abdi Godane ndiye kiongozi wa kundi hilo ambaye wakati
mwingine hujulikana kama Mukhtar Abu Zubair, na anatoka katika jimbo la
Somaliland.
Kumekuwa na taarifa za mgawanyiko katika kundi hilo, ambazo
hata hivyo zinapingwa vikali na kundi lenyewe.
Inaelezwa kuwa uongozi wake unapingwa, na wanachama
wanaotoka maeneo ya Kusini na ambao ni wengi katika kundi hilo ambao wanadaiwa idadi
yao kuwa ni kati ya wanajeshi 7,000 na 9,000.
Godane huwa haonekani hadharani kama ilivyokuwa kwa mtangulizi
wake, Moalim Aden Hashi Ayro, aliyeuawa katika shambulizi lililofanywa na
Marekani mwaka 2008.
Mahusiano yake
kimataifa
Al-Shabab lilijiunga na al-Qaeda Februari mwaka 2012 na hilo
lilibainishwa katika ujumbe wa Video uliooneshwa kiongozi wa al-Shabab Ahmed
Abdi Godane akisema anaahidi kuunga mkono kingozi wa al-Qaeda Ayman
al-Zawahiri.
Makundi hayo mawili yamekuwa yakifanya kazi kwa pamoja, na
raia wa kigeni wamekuwa wakiunga mkono kundi hilo, na hata kuwasaidia katika
harakati zao za mapigano.
Mwaka jana maofisa wa al-Shabab waliambatana na mtu
aliyesema ni mwanachama wa al-Qaeda na kumtambua kuwa raia wa Marekani Abu
Abdulla Almuhajir alipokuwa anatoa msaada wa chakula kwa waathiriwa wa njaa.
Maofisa nchini Marekani wanaamini kuwa wapiganaji wa Al
Qaeeda waliokuwa Afghanistan na Pakistan wamekuwa wakitafuta hifadhi katika nchi
ya Somalia.
0 comments:
Post a Comment