Social Icons

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sunday, October 6, 2013

Makomando wa Marekani wachemka kuishambulia Al Shabaab

MOGADISHU, Somali
MAKOMANDO wa Marekani wameingia nchini hapa na kufanya mashambulizi katika jengo lililokuwa likiaminiwa kukaliwa na kiongozi wa kundi la Al Shabaab.
Mashambulizi haya yamefanyika ikiwa ni wiki kadhaa baada ya kundi hilo kushambulia jengo la kibiashara la nchini Kenya la Westgate.
Kundi la makomando la nchini Marekani limeelezwa kufanya shambulizi katika Pwani ya mji wa kusini mwa Somalia dhidi ya wapiganaji hao wa al Shabab.
Shambulizi hilo lililenga kumuua kamanda wa ngazi za juu wa wanamgambo hao wa kundi la Al Shabab aliyetajwa kwa jina la Abu Siyad anayeishi katika mji wa Baraawe.
Hayo pia yamethibitishwa na Waziri wa Mashauri ya nchi za Nje wa Marekani, John Kerry aliyesema kuwa mashambulizi hayo yamefanywa na wanajeshi wa kikosi maalumu cha Marekani nchini Libya na Somalia yanaonesha dhamira ya serikali ya Marekani kuwasaka wale wanaohusika na ugaidi.
Naye ofisa mmoja wa jeshi la Marekani amekiri kuwa vikosi hivyo vya Marekani havikufanikiwa katika shambulizi hilo la kumuua kiongozi wa Al Shabaab.
Maofisa wa Marekani wamesema kuwa shambulizi hilo lilipangwa wiki moja na nusu iliyopita kutokana na kuchochewa na hujuma iliyofanywa na wanamgambo wa al Shabab dhidi ya jengo la kibiashara la Westgate jijini Nairobi mwezi uliopita.
Mashambulizi hayo yamethibitishwa pia na msemaji wa kundi la al Shabab Abdulaziz Abu Musab aliyesema kuwa makomando wa kigeni walivamia Pwani ya mji wa Baraawe kwa kutumia boti mbili za kasi na kuanza kushambulia lakini hawakufanikiwa kufikia malengo yao.
Amesema kuwa baada ya kushindwa kwa shambulio hilo iliwabidi Al shabaab wafanye mashambulizi makali yaliyosababisha askari wa Marekani kukimbia baada ya kuzidiwa.
Taarifa nyingine zinasema kuwa katika shambulizi hilo nyumba moja ilibomolewa katika mji Barawe unaodhibitiwa na wapiganaji wa Al-Shabaab kusini mwa Somalia.
Habari zinaeleza kuwa sababu za kushambuliwa kwa nyumba hiyo zilichangiwa na kufikiri kwamba alikuwamo kiongozi wa kundi la Al Shabaab kutokana na kulindwa na wapiganaji wa kundi hilo.
Redio ya Mogadishu ilielezea shambulizi hilo lililodumu kwa muda wasaa moja lilitokea jana usiku kwa kutumia ndege za kigeni ikiwamo pamoja na askari wa maji.

Mji wa Baraawe uko kilomita 250 kusini mwa mji wa Mogadishu, umekuwa ukidhibitiwa na wapiganaji wa al-Shabaab kwa miaka kadhaa na umekuwa ukishuhudia mashambulizi ya mara kwa mara kutoka kwa vikosi vya kigeni. 

0 comments:

 

Sample text

Sample Text

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sample Text