Rais Obama awaangukia wabunge Republican kupitisha
Bajeti
WASHINGTON, Marekani
RAIS wa nchini hapa Barrack Obama amesema kuwa yuko
tayari kuzungumza na wabunge wa Republican kuhusu kupitishwa kwa bajeti muhimu
ili kurejesha huduma za serikali zilizokwama tangu wiki iliyopita.
Uamuzi wa Rais Obama unaonekana kutaka kuondoa
doa lililopangwa kuwekwa kwenye uongozi wake katika nyanja ya kiuchumi.
Kauli hiyo imetoka baada ya wiki iliyopita, kuripotiwa
kuwa maelfu ya wafanyakazi wa Serikali nchini humo walirudi majumbani baada ya
kukosa kazi kwa kutokuwepo kwa fedha za kufanikisha huduma muhimu za serikali
baada ya wabunge wa Republican kukataa kupitisha bajeti hiyo muhimu.
Wabunge wa Republican wakiongozwa na Spika wa
Congress John Boehner wamesema kuwa wao wako tayari kwa mazungumzo lakini walisikitishwa
na hatua ya rais Obama kukataa kuzungumza nao.
![]() |
| Rais obama |
Boehner ameongeza kuwa hatua ya rais Obama
kuwataka wao kujisalimisha na kukubali sera zake ni hatari kwa uchumi wa
Marekani ambao huenda ukadorora ikiwa suluhu halitapatikana kufikia Oktoba 17,
mwaka huu kwa sababu serikali itafikia mwisho wa kukopa fedha.
Rais Obama kwa upande wake amemjibu Spika
Boehner kwa kumwambia kuwa ana uwezo wa kufungua huduma za serikali kwa
kuruhusu wabunge wa Congress kupiga kura kuamua ikiwa wanataka huduma za
serikali zirejelewe au la.
Wabunge wa Republican wanasema kuwa walichukua
hatua hiyo, ili kuchelewesha sera ya raia Obama kuhusu bima ya afya, mpango
ambao rais Obama ameendelea kusisitiza kuwa hautabadilishwa.

0 comments:
Post a Comment