AU na mipango ya kumuokoa Kenyatta,
Ruto ICC
ADDIS ABABA, Ethiopia
TANGU
alipotangaza nia ya kuwania wadhifa wa urais wa nchini Kenya, Rais Uhuru
Kenyatta na Naibu wake, William Rutto, walijikuta wakibanwa zaidi na hoja ya
mashtaka ya mauaji baada ya uchaguzi wa nchi hiyo mwaka 2007, yaliyokuwa
yamefikishwa mbele ya Mahakama ya kimataifa ya Makosa ya Jinai(ICC).
Wengi
walikuwa wakijiuliza ni kwa namna gani viongozi hao wangeweza kuongoza nchi
hiyo wakati upande mwingine wa sarafu waandamwa na mashtaka katika kesi yao
iliyofunguliwa Hague, Uholanzi.
| Rais Kenyatta (kushoto) na William Ruto |
Raila
Odinga aliyepata kuwa Waziri Mkuu na mpinzani mkuu Muungano wa Jubilee uliokuwa
umewapa ridhaa viongozi hao alikuwa akionesha wasiwasi wake waziwazi na mara
kadhaa ikiwamo kwenye mdahalo wao alisema bila kutafuna neno kwamba itakuwa
vigumu kwa Uhuru Kenyatta kuongoza Kenya wakati akiwa kizimbani na pia itakuwa
ngumu kuongoza kwa kupitia mtandao wa Skype (mawasiliano ya mtandao kwa njia ya
video).
Mara
kadhaa rais Uhuru Kenyatta alipokuwa akitafuta kura amekuwa akiahidi Wakenya na
dunia kwamba kesi yake inayomkabili haitaathiri shughuli za kiuongozi kwani
atakuwa akitumia muda wake wa ziada kujisafisha mbele ya mahakama hiyo ya ICC.
Lakini
cha kushangaza filamu hii ya ICC inajikuta inahitimishwa katika wiki hii kwa
Uhuru Kenyatta kuonesha wazi wazi kwamba hayuko tayari kuandika historia ya
kuwa kiongozi wa kwanza katika ngazi ya urais kutinga kwenye mahakama hiyo
kujibu mashtaka yake ya Jinai.
Kauli
alizozitoa kabla ya kuanza kwa mkutano wa Umoja wa nchi za Afrika(AU),
ziliashiria kabisa hana mpango wa kwenda Hague, Uholanzi kwa ajili ya kujibu
mashtaka yanayomkabili.
Katika
hotuba yake Rais Kenyatta ameishutumu mahakama ya ICC kwa kusema si chombo cha
kutekeleza uadilifu bali ni mahakama ya kibaguzi na mwanasesere wa madola ya
kibeberu.
Akaishutumu
ICC kwa kusema ni wakala wa himaya ya kibeberu anayoiona kama chombo
kinachosambaratika.
Anasema
“Hata ingawa tuliongozwa na kudhibitiwa na mabeberu kwa maslahi ya kikoloni
katika miaka iliyopita hivi sasa sisi ni mataifa yaliyo na huru na hatima yetu
iko mikononi mwetu, na jambo muhimu kuliko yote ni kuwa macho dhidi ya mifumo
inayoendelea kuwekwa na watu wa nje, wenye nia ya kuidhibiti hatima hiyo”.
Katika
hotuba hiyo Kenyatta ameipongeza AU, kwa kumuunga mkono akisema “Nikiwa kama
Rais wa Kenya, ninastahili kujivuna kwa kuwa naweza kuutegemea Umoja wa Afrika
kwa kunisikiliza na kunisaidia wakati wa matatizo na pia naamini Afrika ipo
pamoja nami”.
Rais
Kenyatta ambaye anakabiliwa na tuhuma za kufanya jinai dhidi ya binadamu katika
mahakama hiyo na amekishutumu chombo hicho kwa kufanya kazi kwa mujibu wa matakwa
na maamuzi ya nchi za Ulaya na Marekani dhidi ya nchi zinazojitawala na mataifa
ya Afrika.
Kiongozi
huyo kwa kuonesha kwamba hatarajii wala hana mpango wa kwenda kujibu mashtaka
yake Hague kama aliovyokuwa ameahidi hapo mwanzo alisema hayuko taari kujisalimisha
katika mahakama hiyo.
Nyundo zaidi
ya kuonesha kwamba kiongozi huyo hatakwenda kujibu mashtaka hayo ilipigiliwa na
viongozi wa Afrika waliokutana Addis Ababa ambao kwa kauli moja waliitaka
Mahakama ya Kimataifa ya Jinai kuahirisha kesi ya Rais Kenyatta na Makamu wake
William Ruto.
Uamuzi wa
mkutano huo ulimpa kichwa zaidi kwa kulitaka Baraza la Usalama la Umoja wa
Mataifa kutekeleza kifungu nambari 16 cha mkataba wa Roma ambacho kinaruhusu
chombo hicho kuahirisha kesi, uchunguzi au kukamatwa kwa mtuhumiwa kwa kipindi
cha mwaka mmoja ambao unaweza kuongezwa baada ya kumalizika.
Sababu ya viongozi
hao kufikia katika makubalino hayo inatokana na ukweli kwamba viongozi walioko madarakani hawapaswi kuhudhuria mbele
ya mahakama ya ICC.
Viongozi
hao wa Afrika wanalalamikia ICC kwa kusema kuwa wamekuwa wakilenga bara la
Afrika katika kesi zake.
Hayo
yanajiri wakati ambao kesi ya Rais Kenyatta inatarajiwa kuanza Novemba huku kesi
dhidi ya Makamu wake William Ruto tayari inaendelea katika mahakama ya ICC, The
Hague.
Pamoja
na kwamba AU imeunga mkono azimio linalosema kuwa hakuna kiongozi yeyote wa
nchi barani Afrika atakayefika katika mahakama ya kimataifa lakini suala la
kujiondoa kutoka ICC lilikosa uungwaji mkono wa kutosha na viongozi wengi.
Katika
mkutano huo wa AU, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia ambaye pia ni mwenyekiti
wa baraza kuu la AU, Tedros Adhamom Ghebreyesus, amekiri kuwa AU haina mamlaka
ya kumzuia kiongozi wa taifa lolote kushtakiwa mjini The Hague akiwamo Kenyatta,
ila wanachopanga kufanya kumsaidia rais huyo ni kuwasiliana na Baraza la
Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kulitaka ili licheleweshwe kabla ya mashtaka
yake kuanza rasmi Novemba 12.
Anaeleza
kuwa Baraza hilo la Usalama ndilo lenye mamlaka ya kuamuru kesi hiyo
kucheleweshwa kwa mwaka mmoja na endapo itaona kuna uwezekano wa kuongeza muda
zaidi litafanya hivyo.
Ghebreyesus
amesema kuwa kama ombi lao halitafanyiwa kazi, AU itaomba kesi dhidi ya
Kenyatta iahirishwe na kama hilo halitafanyika basi viongozi wa Afrika wataamua
kwa pamoja kumzuia rais Kenyatta kufikishwa katika mahakama hiyo mjini The
Hague.
Waziri Mkuu
wa Ethiopia Hailemariam Desalegn, amesema kuwa katika maamuzi yao wameamua Kenyatta
na Rais wa Sudan Omar al-Bashir ambaye pia anatakiwa na ICC kujibu makosa yake
ya uhalifu wa kivita naye hatahudhulia katika mahakama hiyo wakati huu ambao
bado yuko madarakani.
Baada ya
kumalizika kwa mkutano huo wa AU, mara moja makundi ya kutetea haki za
binaadamu, kutoka Kenya na maeneo mengine yalipingwa vikali.
Kwa upande
wa Kenya Naibu mkurugenzi mkuu wa Tume ya Kutetea Haki za Binadamu nchini humo
(KHRC) Davis Malombe amezungumzia wito wa AU kutaka kesi hiyo icheleweshwe.
Malombe
anasema “Hili ni jaribio jingine la kuvuruga na kuchelewesha haki kwa
waathiriwa wa Kenya na unasaliti madai ya ahadi ya AU ya kupambana na ukwepaji
sheria”.
Rais
Kenyatta pamoja na naibu wake William Ruto, wanakabiliwa na mashitaka ya
uhalifu wa kivita kutokana na vurugu zilizofanyika mwaka 2007 na zaidi ya watu
1,000 waliuawa na wengine wengi kuachwa bila makazi.
0 comments:
Post a Comment