Social Icons

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Thursday, October 31, 2013



Operesheni ya kuwaondoa M23 yakamilika

KINSHASA, DRC
MAOFISA wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo(DRC), wametangaza kuwa jeshi la nchi hiyo limedhibiti ngome ya mwisho ya waasi wanaoungwa mkono na Rwanda (M23) mashariki mwa nchi hiyo, hatua inayotia matumani ya kumalizika uasi wa miezi 18 wa kundi hilo.
Msemaji wa serikali ya DRC Lambert Mende amewaeleza wanahabari kuwa mafanikio hayo ya jeshi la serikali kwa sasa yatakuwa yanatoa nafasi ya kuendelea kwa mazungumzo ya amani kati ya kundi hilo na wajumbe wa serikali.
Ripoti zinasema kuwa, waasi wa M 23 waliokuwa wanapiga kambi katika ngome yao ya kijeshi ya Bunagana wanaelezwa kutorokea kusikojulikana huku kiongozi wa kundi hilo Betrand Bissimwa akiripotiwa kukimbilia nchini Uganda nchi ambayo imekuwa ikihusishwa na kuwasaidia waasi hao.
Serikali ya Uganda imethibitisha kuwa Bissimwa yuko nchini humo baada ya kuitwa na msuluhishi Mkuu wa mazungumzo ya amani kati yao na serikali ya DRC Crispus Kiyonga.
Mwakilishi wa serikali ya Kinsasha katika mazungumzo hayo ya amani Francois Muamba, amedokeza kuwa ikiwa kundi la M 23 litakubali mapendekezo waliyotoa basi kuna matumaini kuwa suluhu itapatikana mapema.
Rais Joseph Kabila amesema kuwa bado kuna nafasi ya upatikanaji wa suluhu kupitia mazungumzo ya kisiasa na diplomasia na waasi hao na hivyo wanastahili kuweka silaha chini au wataendelea kushambuliwa kijeshi.
Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa (MONUSCO) katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Martin Kobler mapema wiki hii alilieleza Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa kundi la waasi la M 23 sio tishio tena kijeshi Mashariki mwa nchi hiyo.
Kobler alieleza kuwa waasi wa M 23 wametoroka katika kambi zao za kijeshi na sasa wanajificha karibu na mpaka wa Rwanda baada ya kuelemewa na wanajeshi wa DRC wanaosaidiwa na wale wa Umoja wa Mataifa.
Mapigano kati ya waasi na majeshi ya serikali yalianza wiki iliyopita baada ya mazungumzo ya amani kuvunjika jijini Kampala Uganda na kufikia siku ya Jumatatu hali iliyolifanya jeshi la serikali kupambana nao na kufanikiwa kuchukua miji ya Rutshuru, Kiwanja na Rumangambo yote ambayo hapo awali ilikuwa inadhibitiwa na waasi hao kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Kuondolewa kwa waasi hao kwa mujibu wa mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini DRC ni ishara tosha kuwa waasi hao wamedhoofishwa kijeshi na huenda huu ndio ukawa mwisho wao.
Hata hivyo, waasi hao wa M 23 wanasema kuwa wamejiondoa katika ngome zao kwa muda tu ili kuuonesha ulimwengu kuwa wao hawataki vita kwa mujibu wa rais wa kundi hilo Betrand Bissimwa.

0 comments:

 

Sample text

Sample Text

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sample Text