
Ray C: Juhudi za Rais JK ziungwe mkono
Na Shehe Semtawa
MSANII wa muziki wa kizazi kipya
Rehema Chalamila ‘Ray C’ amwewataka viongozi mbalimbali nchini kuunga mkono juhudi
za Rais Jakaya Kikwete za kupambana na kutokomeza janga la uingizaji na
utumiaji wa mihadarati kwa vijana.
Ray C, aliyabainisha hayo jijini Dar es Salaam juzi, alipokuwa
akizungumza na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa (TAMISEMI), Jumanne Sigini, alipotembelea Kituo cha Tiba cha Dawa za
Kulevya (Methadone Wing).
Alisema anaamini kuwa endapo viongozi waliokabidhiwa dhamana wataziunga
mkono kwa dhati juhudi hizo zilizoanzishwa na rais za kupambana na janga hilo,
anaamini mafanikio ya kulitokomeza yanaweza kupatikana haraka.
“Leo tarehe nane natimiza mwaka tangu nianze kutumia methadone hivyo
nimeamua kufanya sherehe ndogo na wenzangu
‘Rafiki’ katika kituo hiki, nimenunua vinywaji baridi na vitafunwa
kidogo kwa ajili ya kufurahi pamoja”alisema Ray C.
Aidha, Ray C, aliitaka serikali kuongeza jitihada za mapambano yake kwani
janga hilo ni kubwa nchini kutokana na ukweli kwamba wapo hata baadhi ya vigogo
wanaotumia uraibu huo.
“Sasa najisikia vizuri na mshukuru baba (Rais), kwa kunishauri pamoja
na jitihada zake za kuwaleta Wamerekani katika kutupatia tiba hii ambayo
imenirudisha katika hali yangu ya kawaida hadi nikaweza kuingia tena studio
kurekodi nyimbo tena ni jambo kubwa sana”alisema Ray C.
Alitoa rai kwa wasanii wenzake, na baadhi ya watu maarufu ambao
anaamini wapo na tayari wamekwisha athirika na utumiaji wa mihadarati kuwa
wasione aibu wajitokeze katika kituo hicho kwani dawa ya methadone inaponesha,
“Wafike tu watapona kama mimi”alisisitiza Ray C.
Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Sagini, aliiagiza Manispaa ya Kinondoni
kuangalia uwezekano wa kuwapatia ajira baadhi ya vijana hao kutokana na elimu
waliyonayo kwani katika kundi hilo walikuwepo hata wasomi wa elimu ya chuo.
Dk. Elias Mrita, alisema hadi sasa kunawagonjwa 375 ambao hupatiwa
matibabu, na wapo ambao tayari wamekwishapona, aliongeza kuwa kituo hicho
kinaendeshwa kwa msaada wa serikali ya Marekani.
0 comments:
Post a Comment