Social Icons

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Thursday, November 14, 2013



Sitaki kuiona chadema ikifa kizembe

Dk. Slaa nyuma akiteta jambo na Freeman Mbowe, Zitto Kabwe
UNAPOZUNGUMZIA chama ambacho kwa sasa ni gumzo na kinaipeleka puta Chama Cha Mapinduzi (CCM), na kuwafanya viongozi wake washindwe kunywa maji na kukosa usingizi si kingine bali ni chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Lakini katika siku za hivi karibuni nimeanza kupata shaka kuhusu muenendo wa chama hicho kutokana na hali ya kutoelewana ambayo imeanza kujitokeza kwa baadhi ya vijana wake ambao wamekuwa na mvuto mkubwa kwa Wapenzi na mashabiki wa chama hicho.
Ingawa wengi wamekuwa hawazipatii uzito unaostahili chokochoko hizo kwa kuhakikisha wanazitafutia ufumbuzi mpaka inafikia mahali misuguano hiyo inatoka ndani ya chama na hatimaye kuwafikia wananchi kwa kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii hii ni hatari.
Sitaki kuamini kwamba ni vibaya watu kufikia kuwa na migongano ya mawazo, lakini pindi inapofikia mahali migongano hiyo inatoka nje ya vikao halali vya chama huwa ni hatari kwa mustakabari wa chama husika na mageuzi kwa ujumla.
Naamini bado Watanzania tulio wengi hatujasahau kilicho tokea kwenye chama cha NCCR- Mageuzi chama kilichoaminika kuwa mzizi Mkuu wa mageuzi nchini miaka ya 1990.
Chama hiki kilitokana na kamati iliyoundwa Juni 12, 1991, wakati huo ikijulikana kama National Committee for Constitutional Reform ama kwa kifupi NCCR, ambayo Februari 15, 1992 iligeuzwa kuwa chama cha siasa, kilichoitwa National Convention for Construction and Reform-Mageuzi (NCCR-Mageuzi).
Chama hicho kilipata nguvu ya ajabu katika uchaguzi wa mwaka 1995, Lakini siku zilivyopita, chama hicho kilikumbwa na mgogoro kwa viongozi wake kutofautina kimtazamo, ambapo Marando aliingia katika mgogoro na Mwenyekiti wake wa wakati huo, Augustine Mrema.
Hali hiyo ilifanya chama kikagawanyike kwa kundi moja lililokuwa na wajumbe wengi wa Kamati Kuu likimuunga mkono Marando huku Mrema akiwa na wanachama wengine waliokuwa nyuma yake.
NCCR-Mageuzi ikagawanyika kwa makundi mawili ambako kundi la Marando lilihama kutoka ofisi za Makao Makuu zilizokuwa eneo la Argentina, Manzese na zikafunguliwa mpya maeneo ya Posta mpya jijini Dar es Salaam.
Mgogoro huo uliendelea hadi katika Mkutano Mkuu wa chama hicho uliofanyika katika hoteli ya Raskazone mkoani Tanga, ambapo vituko vilitawala, vikiwemo vipigo na vitisho vya kuuana na hata Mrema alipoona NCCR-Mageuzi yamemshinda, aliondoka katika chama hicho na kujiunga na Chama cha Tanzania Labour (TLP).
Hayo ni baadhi ya mambo ambayo nilitaka kukumbusha kidogo, ili iwe fundisho kwa Chadema ambao wamekuwa wakiona kila linalotokea na kulidharau hivyo sitaki kuona yanawakuta yaliyokipata Chadema.
Mgogoro unaoendelea hivi sasa ukiwahusisha Zitto Kabwe na Godbless Lema usichukuliwe kijujuu na kudharauliwa yasije yakawakuta yaliyokikuta NCCR-Mageuzi.  
Hali iliyonifanya nione mgogoro huo unaweza ukatoa taswira mbaya ni taarifa ambayo Zitto ameitoa hivi karibuni akijaribu kujibu taarifa inayoelezwa kutolewa na chadema ikiwa na kichwa cha habari "Taarifa ya Siri ya Chadema"
Sehemu ya taarifa hiyo anasema nilipokuwa katika ziara ya bara la Ulaya kati ya Oktoba 21 mpaka Novemba 2 mwaka huu, nilipokea kwa njia ya barua pepe ripoti inayoitwa "Taarifa ya Siri ya Chadema" ambayo pia ilikuwa imesambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii.
“Taarifa ya Chadema inasema kwamba chama hicho (chama changu) kilikuwa kimechunguza mwenendo wangu tangu mwaka 2008 hadi 2010 na kubaini kuwa mimi napokea fedha kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuivuruga Chadema.
Ripoti hiyo ilinihusisha pia na mwananchi raia wa Ujerumani, Andrea Cordes ambaye, kwa mujibu wa ripoti hiyo, alinisaidia kupokea na kuhifadhi kiasi cha dola 250,000 za Marekani kupitia kwenye akaunti yake binafsi. Taarifa hii ya kutunga na iliyojaa uongo wa kiwango cha kutisha, imenifadhaisha, kunisikitisha na kunikasirisha.
Taarifa hii iliibuliwa katika kipindi ambacho nilikuwa safarini kutetea haki za Watanzania na Waafrika ambao utajiri wao wa rasilimali unafaidiwa na watu wachache waliohifadhi mali katika nje za nje na pia kupigania makampuni ya mataifa tajiri yalipe kodi stahiki katika nchi zetu.
Pengine lengo la ripoti hiyo lilikuwa ni kutaka kunipoteza kutoka katika nia na dhamira yangu ya dhati ya kutaka Watanzania wafaidike na utajiri wao. Muda ambao watunzi wa ripoti hiyo waliamua kutoa taarifa yao unazua maswali mengi kuliko majibu.
Nafahamu kwamba mimi ni mwanasiasa ambaye nimekuwa mlengwa (target) wa mashambulizi kutoka kwa makundi mbalimbali ya wanasiasa na vikundi vyao. Kama mwanasiasa, niko tayari kupokea changamoto zozote zinazokuja na uanasiasa wangu.
Hata hivyo, ambacho sitakubali ni kwa watu kutumia jina langu na uanasiasa wangu kunichafua mimi binafsi na watu wengine wasiohusika kwa sababu ya kutaka kutimiza malengo yao ya kidhalimu.
Raia huyo wa Kijerumani tayari amekana kuhifadhi fedha zangu. Kwa maelezo yake kwa baadhi ya viongozi wa Chadema amekana kuwa na akaunti inayotajwa na amekana pia kuwepo nchini Ujerumani katika siku na wakati uliotajwa kwenye ripoti hiyo.
Ripoti hiyo imemtaja pia Dk. Charles Kimei, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB ikidai kwamba nilikutana naye na alishiriki kwenye igizo hilo la kunipa fedha.
Niseme mapema kwamba tangu kuzaliwa kwangu sijawahi hata mara moja kukutana na Dk. Kimei popote pale ndani au nje ya nchi. Kumuingiza mtu ambaye amejenga jina lake kwenye taaluma ya kibenki kwa sababu tu ya lengo ovu la kumchafua Zitto Zuberi Kabwe si uungwana bali ni unyama.
Kutokana na uchafuzi huu wa wazi dhidi ya taswira yangu binafsi na watu wengine walioingizwa kwenye mkumbo huu, nimeandika rasmi kwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk.Wilbrod Slaa kumwomba athibitishe kwamba kinachoitwa Taarifa ya Siri ya Chadema ni kweli ni taarifa ya chama au kiikanushe ili niweze kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waandishi wa hekaya hiyo.
Cha ajabu, nimepokea ujumbe wa kutishiwa maisha kutoka kwa mtu anayejiita Theo Mutahaba na kuahidiwa kupotezwa endapo nitaendelea na jitihada zangu za kupambana na ufisadi na kutafuta haki kwa Watanzania wote pasipo kujali tofauti zao za kiitikadi, kikanda, kikabila na kidini.

0 comments:

 

Sample text

Sample Text

PATA HABARI NA BURUDANI MBALI MBALI POPOTE ULIPO!

Sample Text