M23 wagawanyika mkataba wa amani DRC
KINSHASA,
DRC
![]() |
| M23 |
KUNDI la waasi
wa M23 la nchini hapa limeelezwa kugawanyika kuhusu kushindikana kwa utiliwaji wa
saini mkataba wa amani kati yake na Serikali ya Kinshasa.
Hatua hiyo
imefikia siku chache baada ya kuvuinjika kwa mazungumzo yaliyofanyika jijini Kampala
yavunjike kwa kushindwa kutiliana saini hati ya makubalino waliyofikia kati ya
wajumbe wa serikali ya DRC na kundi la M23.
Taarifa
kutoka mjini Kampala zinasema kuwa kuna kundi jingine ambalo limejitenga kutoka
kundi la waasi wa M23 ambalo lenyewe linaunga mkono mapendekezo yaliyokuwa
yametangazwa na Serikali.
Taarifa
iliyotolewa na kundi lililojitenga na M23, inasema kuwa wao hawaungi mkono
madai ya wenzao na badala yake wanataka kukubaliana na Serikali ya DRC kuhusu
kutiliana saini azimio la amani kwa mustakabali wa Wananchi wa Kongo.
Taarifa hiyo
iliyotiwa saini na Serge Kambasu Ngeve anayedai ni katibu mkuu wa kundi
lililojitenga, inasema kuwa wao wako tayari kuzungumza na Serikali ya Kinshasa
katika kutafuta njia muafaka za wao kusalimisha silaha na kutia saini azimio la
amani.
Wakati hayo
yakijiri Umoja wa Mataifa (UN) umeitaka Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Kongo kuandaa mpango kabambe wa kuhakikisha makundi mengine ya waasi
wanasalimisha silaha ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha kwenye jeshi la nchi
hiyo.
Tamko la UN
linatolewa wakati huu ambapo kikosi maalumu cha umoja huo kilichoko mashariki
mwa nchi hiyo ya DRC kwa kushirikiana na wanajeshi wa Serikali (FARDC)
walifanikiwa kuwaondoa wapiganaji wa kundi la M23.
Operesheni
hiyo ilifanikisha kumaliza uasi wa kundi la M23 uliokuwa umedumu kwa zaidi ya
miezi 18 ambapo mamia ya watu wamepoteza maisha na wengine kuyakimbia makazi
yao.
Naibu katibu
wa Umoja wa Mataifa kwa nchi ya Kongo, Abdallah Wafi amewaambia wanahabari kuwa
mpango huo ni muhimu kwa Serikali ya Kinshasa kama njia mojawapo ya kufikia
suluhu ya amani mashariki mwa nchi hiyo.
Baadhi ya
wapiganaji wa kundi la M23 walijisalimisha kwa vikosi vya Umoja huo na wengine
kukimbilia Rwanda kuomba hifadhi jambo ambalo pia huenda likasababisha
wapiganaji waliosalia na ambao hawajasalimisha silaha kujikusanya.
Katika hatua
nyingine jeshi la Serikali ya DR Congo limesema hivi sasa linajipanga kuanza
mashambulizi mapya dhidi ya wapiganaji wa Kinyarwanda wa kundi la FDLR ambao
wakati fulani walipigana na Serikali mashariki mwa nchi hiyo.

0 comments:
Post a Comment